JINSI YA KUWASAIDIA WATOTO WAJE KUWA WAJASIRIAMALI

Wajasiriamali ni watu muhimu sana katika jamii, kwa sababu nyingi kama vile kuongeza ajira, kuongeza bidhaa na huduma, kuboresha maisha ya watu kupitia bidhaa na ajira n.k. Mjasiriamali  ni mtu mwenye kuthubutu kuanzisha shughuli ya uzalishaji, kuboresha utendaji wa namna fulani. Wajasiriamali huamini katika 'ndoto' zao , na hukubali kujishughulisha kwa shughuli zozote wanazodhani zitapelekea 'ndoto' zao kufanikiwa, huku wakiamini pia kuna uwezekano wa wanayoyafanya yasifanikiwe. Hata hivyo hatari hiyo ya kutokufanikiwa, haiwafanyi kuacha wanayolazimika kufanya.
Makala hii inadokeza mambo unayoweza kufanya kwa ajili ya mtoto ili kumuandaa mtoto kuja kuwa mjasiriamali.
1. Kujifunza 'kutengeneza' fedha: Msaidiie mtoto kadri anavyokua na kupata ufahamu wa kutosha awe na utamaduni wa kujiingizia kipato. Mfano unaweza kumpa kazi ambazo akifanya kwa kiwango mnachokubaliana unamlipa fedha. Muweze pia kushiriki shughuli ndogo ndogo za ujasiriamali kama vile kukaa dukani (kama mna duka), kupeleka bidhaa kwa wateja wako, n.k  Hii itamsaidia kujenga ufahamu kuwa fedha inapatikana kwa mabadilishano ya bidhaa/huduma na ataanza mapema kujenga ufahamu wa mbinu, matatizo na michakato ya kijasiriamali. Pengine vinaweza visimsaidie sana akiwa mtoto, ila kadri anavyokuwa, ataweza kuunganisha 'uzoefu' wake.

2.Nidhamu ya fedha: Mtoto anapaswa kuelimishwa kuhusu matumizi ya fedha, ajue na kuweka akiba. Pia kwa nidhamu ya fedha, inapasa mtoto asizoeshwe kupewa fedha kirahisi rahisi, kwani hii haimjengi kufikiria kuhusu 'kutengeneza' fedha, badala yake anazoea 'kudaka', hivyo kumuandaa kuwa muajiriwa wa kudumu.

3. Ulimwengu wa biashara: Ni vizuri kumpatia mtoto ufahamu wa mambo yanavyoenda katika ulimwengu wa biashara, mfano aone vile unavyojadili bei, ajifunze kuhusu huduma kwa wateja, na unapoona hayo unakuwa unampa maelekezo mtoto. Mfano, unapokuwa naye na ukapatiwa huduma mbaya toka kwa mfanyabiashara fulani, mueleze mtoto kuwa hivyo sivyo sahihi katika ulimwengu wa biashara. Muweze mtoto kutembelea maeneo ya uzalishaji kama vile viwandani.
We are what we repeatedly do.- Aristotle
Sisi huwa vile ambavyo mara nyingi tumezoea kufanya.
4. Chochea ubunifu wake: Watoto karibu wote wana aina fulani za ubunifu. Msome mtoto wako, na mpe moyo kwa kila jambo analofanya la ubunifu. Mfanye atambue kuwa unamuamini, na pia mueleze kuwa anaweza kufanya lolote analodhani anataka kufanya la kiubunifu. Msaidie ikibidi kununua vifaa, kumpeleka safari mbalimbali, n.k ili mradi awe huru kubuni. Hapa unamjengea uwezo wa kujiamini.
Imagination is more important than knowledge.-Albert Einstein
Kufikiria/mawazo ni bora kuliko ufahamu
5. Mawasiliano na mtoto: Watoto wanatabia ya kuamini zaidi wazazi au walezi wao. Hivyo una nafasi kubwa ya kumjenga mtoto kuwa mjasiriamali kwa kufanya nae mazungumzo ya mara kwa mara. Mfundishe kuwa na mikakati. Muulize anapenda kufanya nini, muulize anapanga kufanya nini katika muda wake wa mapumziko, n.k. Pamoja na ugumu wa maisha unaowafanya wazazi na walezi wengi kukosa muda na watoto, hakikisha unatenga muda kwa ajili yake, kwani wewe ni mchochezi mkubwa wa namna maisha yake ya baadae yatakavyokuwa.

6. Mwezeshe kujisomea: Bila kusahau , tambua ubunifu ni nguzo kubwa katika ujasiriamali, na ili kuwa na ubunifu, mtu anapaswa kuwa na taarifa /ufahamu mkubwa wa mambo kwani ufahamu huo ndio unamuwezesha kutambua yapi yanawezekana na yapi hayawezekana, na hapo ndipo anapokuja kuona 'gap' iliyopo ili kuziba hiyo 'gap'.
Hivyo basi , mjengee mtoto mazoea ya kujisomea. Muwezeshe ajue lugha vema hususani lugha ya kiingereza.

Hitimisho:
Haijalishi aina gani ya fani mtoto atakuja kufanya kazi hapo baadae, awe mwanamichezo, mwanasheria, mhandisi, mhasibu, daktari , n.k, uwezo wa kufikiria kijasiriamali, uwezo wa kutaka kuzalisha zaidi, ni muhimu kwake na kwa jamii. Na zaidi sana, ajira atakayopata hapo baadae itamsaidia kujiingizia kipato ambacho kitamuwezesha kukusanya mtaji wa kujiajiri.
Kuna msemo mzuri toka kwa Peter F. Drucker:
“This defines entrepreneur and entrepreneurship - the entrepreneur always searches for change, responds to it, and exploits it as an opportunity.”
Hivyo kumsaidia mtoto kuwa mjasiriamali kuna faida kubwa zaidi kuliko kumuacha hivyohivyo. Anza sasa.
Share:

0 comments:

Post a Comment