MAMBO 5 YANAWEZA SAIDIA KUTIMIZA NDOTO ZAKO

Ni muhimu kuwa na utamaduni wa kuheshimu  ndoto zetu hata kama tunadhani kuwa ni ndoto ndogo kama vile ndoto ya kutembelea mkoa fulani, ndoto ya kutembelea nchi fulani, ndoto ya kumiliki aina fulani ya mali, n.k. Hata hivyo, kuweza kuheshimu ndoto zetu na kuzitimiza, kunahitaji nidhamu ya ziada, ingawa wapo wanaozifikia ndoto zao kwa bahati.
Wengi husema wanataka kutimiza ndoto zao, hata hivyo ni wachache hufanikiwa kutimiza ndoto zao. Kwa kuwa binadamu tuna ndoto tofauti tofauti, ni ngumu kuwa na kanuni moja ya jinsi ya kufikia ndoto zetu, hata hivyo uzoefu unaonyesha mambo kadhaa ambayo watu wengi waliofikia ndoto zao wamefanya. Mambo haya ndio tunayojadili katika makala hii:-

1. Ota ndoto kwa usahihi: Kuota ndoto ya mabadiliko ya maisha yako, sio tuu kuwaza au kutamani kufikia hali fulani, bali kuota kwa usahihi ni kutengeneza picha kichwani ya hali unayotaka kufikia, au mambo unayotaka kuyapata. Na zaidi sana, itengeneze picha ya hali unayotaka kufikiaau mambo unayotaka kufikia katika mawazo yako kiasi kwamba ufikie hatua ‘unahisia za kuwa tayari umefikia hali unayotaka au umeyapata hayo unayoyaota. Ikiwezekana weka katika maandishi ndoto zako ili iwe rahisi kuzikumbuka mara kwa mara.  

2. Tafakari kwa umakini: Ukishaipata kwa uhakika ndoto yako au ndoto zako, endelea kutafakari ili kutambua kwa undani  ili kutambua mambo ya msingi kuhusu ndoto yako kama vile:-
  • Mambo gani utatakiwa kufanya (Mfano kiwango cha elimu, kujua lugha za kigeni, kupata uzoefu fulani, n.k)
  • Aina ya mazingira yanahitajika ili kufikia ndoto hiyo (Mfano: Kupata washauri, Kujenga mtandao wa aina fulani ya watu n.k)
  • Kiasi gani cha juhudi au bidii inabidi uwe nayo ili kufikikia ndoto huto zako. (Mfano: Mazoezi ya kila siku, kujaribu biashara mbalimbali, n.k)
  • Aina gani ya msaada unahitajika (Mfano: Kama unahitaji fedha, unahitaji mtu wa kufundisha mambo fulani)

3. Weka mkakati: Mikakati ni yale yote unayoweza kufanya ili kufikia ndoto zako. Kupitia tafakari uliyoifanya kama ilivyoelezwa hapo juu, utaweza kupanga mbinu na namna ya kuzitekeleza mbinu za kufikia ndoto yako.

4. Amini na uwe mvumilivu: Tambua kuwa baadhi ya ndoto huchukua muda kutimia. Na pia sio juhudi zote utakazofanya zinaweza kufanikiwa. Hivyo unahitaji kuwa na uvumilivu na imani kubwa katika ndoto zako.  Usichoke pia kuchunguza mara kwa mara mikakati yako ili kuiboresha.

5. Fanya unachotakiwa kufanya kwa bidii na maarifa: Kuwa na ndoto pekee hakufanyi ndoto hizo kutimia. Unahitaji mikakati. Na zaidi sana unahitaji kufanyia kazi mikakati yako. Kumbuka kuwa ingawaje kuna swala la watu kufikia ndoto zao kwa bahati, tambua kuwa bahati ikikufikia wakati ambapo hauna uwezo au mazingira uliyonayo hayakuruhusu kuitumia bahati husika, basi bahati hiyo haitokuwa na maana kwako. 

Hitimisho: Maelezo hapo juu yanahitaji tafakari ya umakini, na utilie mkazo kila hatua. Anza kwa kuandika mambo unayodhani ndio ndoto zako. Usisahau kutembelea mara kwa mara orodha yako ya ndoto, tafakari ni ndoto zipi umefikia , na zile usizofikia tafakari jinsi ya kuzifikia. Nakutakia kila la kheri katika kufikia ndoto zako, najua ni furaha sana kufikia ndoto, hata kaka ni ndoto ‘ndogo’.
Share:

2 comments: