MAMBO 4 YAFANYAYO KUTAKA KUONEKANA ‘UPO JUU’ KUWA NI UTUMWA

Dale Carnegie aliwahi kusema “Kinachokufanya uwe na furaha Sio kile ulicho nacho, au vile ulivyo, au wapi ulipo, au kipi unafanya, bali ni vile unavyofikiria kuhusu hayo yote”. Hata hivyo miongoni mwetu , tumejikuta tuna wakati mgumu wa kujisikia na furaha kwakuwa tumetilia mkazo kufanya mambo kwa ajili ya kuonekana mbele za wengine.
Haijalishi namna gani ‘unauza sura’-yaani unatafuta kuonekana kuwa upo ‘juu’ iwe kwa kujibadili jina, kujidai kwa mavazi, mali kama nyumba au gari, kwa cheo, au kwa watu unaowafahamu, hayo yanaweza kuashiria upo kwenye mkumbo wa hali hii mbaya ambayo ukiitafakari kwa undani utagundua kuwa ina chembe chembe za utumwa wa kifikra.
Kuuza sura au kujidai kama ninavyojadili katika makala hii ni ile hali ya mtu kutaka kuonekana yupo ‘wa hadhi ya juu’ mbele za wengine, kwa lengo kuu la kutaka tuu kuwa juu kama njia ya kukubalika mbele ya jamii au kama njia ya ‘kupata heshima’ toka kwa hao anao walenga.
Kuna matendo mengi ambayo mtu anaweza akawa anatenda akatafsirika kama ‘anauza sura’ ingawa si kweli anauza sura, kwakuwa hana lengo la kutafuta heshima kama heshima, bali kuna malengo mengine ya ziada kama vile malengo ya biashara – kutangaza bidhaa, au kujenga jina lake kwa kutafuta umaarufu n.k.
Kuuza sura tunakokuzungumzia hapa kunaleta mambo yafuatayo:-

1.Tunasahau nini hasa tunahitaji: Tunapotilia mkazo  kujionesha kuwa sisi ni bora zaidi ya wengine kwa sababu za ‘kujidai’ tunajikuta tunaweka mkazo zaidi katika namna vile wengine wanategemea sisi tuwe, au tuseme tunaweka mkazo kwenye mambo yanayoonekana au kukubalika na wengi kuwa ‘ni matawi ya juu’. Hali hii inaweza kutufanya tusiweke mkazo katika tafakari ya mambo ya msingi ambayo sie wenyewe binafsi haswa tunahitaji. Mfano, badala ya kutilia mkazo mahitaji ya familia yako ya sasa, na hapo baadae kama vile elimu, afya n.k unaweza ukawekeza sana kwenye vitu vya kifahari ili na wewe uonekane upo ‘juu’. Ndio maana si ajabu, kusikia msanii maarufu aliye ‘tesa’ , akiombewa msaada wa kugharimiwa gharama za matibabu! Au kijana aliyeonekana miezi michache iliyopita ‘akitesa’, sasa amekuwa ombaomba misaada kwa watu mbalimbali.

2.Tunajiweka katika hali ya kujikataa: Kwa kuwa tayari tumeshakubali kuwa utimilifu wa furaha yetu ni kuwa ‘juu’ zaidi ya wengine, au kupata hisia kuwa wengine wanatuona tupo juu, tunajikuta tunajikataa sie wenyewe pale tunapoona kuwa hatujafikia viwango. Ndio maana si ajabu kusikia mtu akisema anaishi Masaki, wakati kiukweli kwao ni Tandale. Kwa hali hiyo hiyo, ndio maana si ajabu kumkuta mtu akipiga picha kwa nguo za kuazima, au kwa namna ya ubora zaidi itakayo ng’arisha muonekano wake na kuiweka Facebook ili hali, katika muonekano halisi hayupo hivyo.

3.Akili inapumbazika: Mambo mengi yanayotumika na watu kutafuta kuonekana wapo juu,  huwa si mambo halisi, bali ni mambo ya mpito, ambayo pengine watu hufuata mkumbo na kuyatumia isivyopaswa. Mfano, kuna wakati watu walitumia Flash Disks, kama kitu cha kuonyesha ‘wapo juu’, wengi walikuwa wanazibeba bila matumizi, na wakati huo huo, lengo la Flash Disk halikuwa kuonyesha ‘status’ ya mtu.
Mfano mwingine ni simu za mkononi , kuna wakati ilikuwa kuwa na simu ya mkononi ni kuwa ‘upo juu’. Hali kadhalika, siku za hivi karibuni kuwa na gari kumeonekana kama ni jambo la kuuza sura. Cha ajabu zaidi hata kuweka status na kuwa na likes nako kumechukuliwa kama sehemu ya kutengeneza ‘heshima’.
Viwango vya elimu pia vimekuwa vikitumika katika kutafuta ‘status’ wakati ki uhalisia, elimu ina kazi nyingine tofauti na hiyo ya ‘kutia adabu’ watu wengine. Utakuta kwa mfano, mtu akitafuta digrii, au Masters au akifanya uchaguzi wa jina la chuo, sio kwa sababu kuu ya manufaa ya uchaguzi husika bali ni kwa kuangalia namna ambavyo  ‘status’ yake itatafsirika, kuwa na yeye ‘yupo juu’.
Wengine huko Facebook, wamefikia hatua ya kuwa na majina ya ‘ajabu’ kama sehemu pia ya kuleta heshima mbele za wengine- majina kama DE VOS SHIZO NIZO, na kuweka picha za wasanii mbalimbali ni sehemu pia ya kuuza sura !!

4.Tunasahau uwezo wetu mkubwa:Kwakuwa tunajikita kwenye   kutafuta ‘ujiko’ au ‘heshima’ za bandia, na kwakuwa tunajisahau kufuatilia mambo haswa ya msingi tunayohitaji katika maisha yetu, tunasababisha Uwezo wa kuleta mabadiliko tulionao katika dunia hii kuwa umebanwa na mazingira tuliyonayo. Badala ya kufikiria ‘nje ya boksi’ tunajikuta mtazamo wetu wa maisha unajikita tuu ndani ya ‘boksi’ tulilomo, yaani ndani ya mazingira tuliyonayo – kwa kuangalia wenzetu wana nini, wamefanya nini, wanafikiria nini kuhusu sisi, na wanatarajia nini kuhusu sisi.

Hitimisho:
Makala hii haina lengo la kumaanisha kuwa kuwa kufanya mambo makubwa na mazuri kwa ajili yako kama vile kununua nguo nzuri, gari , nyumba , kupiga picha nzuri, kusafiri au kuishi maeneo mazuri ni vibaya, badala yake inapongeza kufanya mambo kama hayo, kwa manufaa ya mtu binafsi, na sio kuvutwa na kutaka kuvutia watu wengine.
Mwanasayansi na mwanahistoria Paul Rosenberg wa Freemanperspective.comkatika makala yake ya The contentment Revolution anasema:kuwa bora kwako si lazima kuwe na maana wengine wapo chini yako. Rosenberg anaendelea kusema kuwa kama tutajitahidi kufanya mambo kwa sababu yanatupendeza sisi, tukawaza zaidi nini tunahitaji basi ni wazi tutajikuta tunapunguza machungu yasiyo ya lazima ( mfano, machungu ya kujisikia upo chini ya watu wengine), na hata kupunguza hasara ya fedha, muda na mambo mengine tunayopoteza ili tuu kuwafanya watu wengine watuone kuwa eti sie tupo juu!.
Nimalizie kwa nukuu hii:

“Usiharibu kile ulichonacho, kwa kutaka kile usicho nacho”. Epicurus
“Do not destroy what you have, by desiring what you don’t have”. Epicurus
Share:

0 comments:

Post a Comment