MAMBO HAYA 6 YANAYOATHIRI UFAHAMU WETU

Vitabu vya dini vinasisitiza tutafute elimu, na katika Biblia (Hosea 4:6) kuna andiko linasema kuwa watu wanaangamia kwa kukosa maarifa. Hivyo basi ni wazi kuwa tukifanya bidii katika kuboresha ufahamu wetu, tutaweza kutatua changamoto nyingi, na  tutaweza kuishi maisha yenye furaha na maendeleo.
Lengo la makala hii sio kusisitiza umuhimu wa kupata maarifa, bali makala hii inalenga kukudokeza mambo ambayo yanaweza kuwa adui yako katika juhudi zako za kutafuta maarifa.
Ifuatayo ni orodha ya mambo 6 kama yanavyotajwa na mtaalamu wa elimu ya jamii Earl Babbie katika kitabu chake “The Practice of Social Research” (2010), 12th edition, ukurasa wa 4-8.
Nimeongeza maelezo ya ziada katika points hizi toka kwa Babbie, ili kuboresha ufafanuzi kwa ajili yako:-

1. Tamaduni zetu: Sote tumejikuta tukiamini aina fulani ya maarifa kutokana na jinsi tamaduni zetu zinavyotuambia , na kwakuwa hivyo ndivyo kila mtu anavyofahamu, basi hatuoni haja ya kuhoji usahihi wa mambo husika, hata kama pengine si sahihi. Ingawa ni kweli kufuata tamaduni ni jambo jema, kuna hasara ya kutufanya tuwe wavivu wa kutafakari zaidi na kutafuta maarifa zaidi, na jambo baya zaidi ni kuwa tamaduni zinaweza kutufanya tukawa waoga wa kutafuta maarifa tofauti, kwani kufanya hivyo tutaonekana kuwa ni ‘waasi’ wa tamaduni. Kumbuka lugha, na dini zote ni sehemu ya tamaduni tulizorithi.

2. Mamlaka: Ni mazoea pia kufuata maarifa ya watu ambao tunawaona ni ‘viongozi’ katika jamii zetu. Wawe ni watu maarufu, wanasiasa, viongozi wa dini, au ‘wasomi’ wa vyuo vikuu. Kwa mpango huu , ni rahisi kwetu kukataa maarifa ya watu ambao hawana ‘mamlaka’ yoyote. Tatizo katika hali hii ya kufuata mamlaka ni kuwa kuna nyakati tunaweza tusipate maarifa sahihi, au tukajikuta hatufuati kweli maarifa kwa sababu ni maarifa bora, bali ni kwa sababu tunaangalia zaidi nani katoa maarifa husika.  Ni rahisi kwa mfano, kumsikiliza na kumuamini kiongozi wa kidini akitoa ushauri wa biashara kuliko kumsikiliza mfanyabiashara mdogo ambaye anao uzoefu wa miaka zaidi ya 10 katika biashara. Pia ni rahisi kuamini na kufuata mambo unayosoma kwa blogu ya mtu maarufu, kuliko kusoma blogu kama hii ya MBUKE TIMES, kwakuwa si ya mtu maarufu.

3. Kutokufuatilia mambo kwa umakini: Mara nyingi huwa tunajikuta tunafuatilia mambo juu juu,hivyo kutokupata taarifa zote na taarifa zilizosahihi. Mbaya zaidi unaweza kukuta mtu akipinga au kushutumu jambo ambalo hajalifuatilia kwa umakini.  Mfano mzuri katika hili ni namna ambavyo tunasoma magazeti au taarifa za mitandaoni. Je, huwa unatumia muda kupata taarifa zote kwa usahihi, kuchunguza kama habari ni muendelezo wa habari nyingine, au itafuatiwa na habari nyingine. Je, unaelewa maneno ya msingi katika makala husika unayoisoma ?. Kutokufuatilia mambo kwa umakini hujitokeza pia hata katika kutazama kwetu, je tunajifunza nini kutokana na mazingira tunayoyaona, rangi, aina ya mavazi , n.k ya watu tunaokutana nao ? 

4. Kutoa maamuzi ya jumla isivyo sahihi: Mara nyingi tumejikuta tukifikia hatua ya kuamini ‘ukweli’ fulani kwa sababu ya  kujirudia rudia kwa jambo, hivyo tukiamini kwakuwa tuu jambo limejirudia rudia mara nyingi, au kwakuwa watu wengi wana mtazamo unaofanana, basi jambo husika ni sahihi kwa watu wote, hivyo maarifa yetu yanajengwa katika imani au mtazamo usio sahihi. Mfano kwakuwa mara nyingi ukiwa na haraka na ukafika kituoni usikute daladala, na kwakuwa jambo hili huwatokea watu wengi, inaweza kusemwa kuwa ‘aah, ukiwa na haraka sikuzote hautokuta daladala kituoni’.  Pia kuna nyakati kutokana na aina ya mazingira tuliyonayo, aina ya watu tunaoishi nao, tunajikuta tukijiaminisha kuwa watu wengine mahali kwingine ni lazima watakuwa na tabia kama hizo. Ubaya wa aina hii ya kujenga maarifa yetu ni kuwa, inatufanya nyakati nyingine kupata maarifa yasiyo sahihi, na inatufanya kuwa wagumu kubadili mtazamo wetu. Chukulia mfano, kuna watu wanaamini kuwa blogu za kibongo hazina habari za msingi zaidi ya siasa, na udaku, na kwamba nyingi habari zake ni copy & paste, na hazijafanyiwa uchunguzi. Kwa imani hiyo, watu hao hawawezi kukuelewa kuwa kuna blogu kama MBUKE TIMES ambayo haipo hivyo wanavyodhani.

5. Kuchagua mambo ya kuchunguza: Kuna nyakati tunajikuta tunafanya uchaguzi wa aina ya mambo ya kutafakari kutokana na misukumo kadhaa katika maisha yetu, iwe kwa sababu ya tamaduni zetu, hasira, furaha, kuzoeana na watu , au taarifa za awali ambazo tunazo kuhusu watu au jambo fulani. Hali hii huwa ni tatizo katika utafutaji wetu wa maarifa sahihi, kwani tayari tunajiwekea kikwazo cha kupata maarifa zaidi. Mfano, kwakuwa umejiaminisha kuwa siasa ni uongo, basi unajikuta hautaki kusikiliza mtazamo wa wanasiasa, hata kama pengine wapo sahihi. Au kwakuwa wewe ni wa chama fulani cha siasa, basi unajikuta hautaki kusikiliza wala kutafakari hoja na mitazamo kutoka upande wengine wa siasa au wale ambao hawafungamani na siasa.

6. Ku ‘reason’ kusiko sahihi: Mara nyingi tunajikuta katika hali ambazo tunashindwa kuzielezea kwa urahisi , hivyo kujikuta tukibuni sababu za kutokea au kuwepo kwa hali husika. Kuna  sababu nyingi za uwepo au kutokea kwa hali fulani fulani ambako kwa kweli sababu hizo si sahihi, endapo utatafakari kwa undani utaona kuna uwezekano mwingine mwingi ambao bado hatujauangalia katika ku ‘reason’ kwetu.
Mfano 1: Utasikia mtu akisema ‘Aaah sawa tuu, niache niwe masikini kwakuwa sote hatuwezi kuwa matajiri, lazima wawepo masikini na matajiri’.  Ku ‘reason’ huku si sahihi kwakuwa kwanza hakuna ufafanuzi wa kutosha kuwa tatizo gani litatokea kama wote tutakuwa matajiri ? . Je, kama watu wote kuwa matajiri ni jambo lenye tatizo, kwanini basi tunaamini katika swala la Ahera /mbinguni, kwakuwa huko, bila shaka masikini hawatokuwepo.
Mfano 2: Utasikia mtu akitetea kutupa takataka  ovyo mjini au tuseme barabarani, kwa kisingizio kuwa anasaidia kutengeneza ajira kwa watu wa jiji !. Hii nayo ni aina ya ‘reasoning’ isiyo sahihi, kwani si kweli kuwa kama jiji litakuwa safi, basi ajira zitapungua, na si kweli kuwa watu wanaopata ajira katika kusafisha jiji, hawawezi kupata aina nyingine ya ajira, kama vile kuzibua mitaro, kutunza bustani, kusaidia kazi nyingine za usafi wa majengo n.k. Zaidi sana, kuna ushahidi wa kutosha kuwa ipo miji ambayo ni misafi, na bado halmashauri za miji hiyo, zimeajiri watu kwa shughuli mbalimbali zikiwemo shughuli za usafi.
Share:

0 comments:

Post a Comment