MALENGO HAYA MANNE (4) YANATOA PICHA YA MJASIRIAMALI WA ‘UKWELI’

Ninaamini kuwa lengo la mwanzilishi wa biashara lina nafasi kubwa sana katika ku ‘shape’ biashara husika itakavyokuwa, kwakuwa  lengo hili ndio huweka picha ya akilini vile mtu alivyo tayari kujitoa kwa ajili ya biashara yake : wateja wake, wafanyakazi na uzalishaji wa bidhaa.
Makala hii inachambua aina kuu nne (4) za malengo ambayo watu huwa nayo wanapoanzisha biashara:- 

1. Kuongeza kipato cha ziada:  Wenye lengo hili pekee hujikita kwenye kuanzisha biashara hususani biashara za msimu, ili mradi kipato kipatikane. 
Mara nyingi huwa hawana mchanganuo wa kina wa biashara husika, na hawajali mambo ya msingi katika usimamizi wa biashara kama vile kuboresha huduma, kuboresha teknolojia wanazotumia katika biashara husika, kuwa na wafanyakazi wenye ujuzi na uzoefu wa kutosha. 
Kwa wenye lengo kuu la kuongeza kipato cha ziada tuu, biashara zao ni jambo la ziada kwao kwani hujikuta wakitegemea mambo mengine kama vile ajira, kipato cha familia, au biashara nyingine.

2. Biashara kama Ajira mbadala: Wenye lengo hili huchukua muda mrefu kupanga jinsi ya kuanzisha biashara husika, na huweka msisitizo kwenye kipato. Ni wachaguzi sana wa aina ya biashara watakayoanzisha, mara nyingi biashara zao sio za msimu. 
Wajasiriamali wa lengo hili, hutazama zaidi kujenga mtandao kama sehemu muhimu katika kufanikisha biashara zao. Kwa watu wenye lengo hili, la msingi kwao ni kuendelea kuwepo katika biashara hata ikibidi kupata faida ndogo au kupoteza wateja wa aina fulani. 
Wana matazamio ya kukuza biashara zao, hata hivyo hukumbwa na tatizo la mtaji na ukosefu wa uzoefu katika biashara husika. 
Ni wagumu kuamini watu wengine (hususani wafanyakazi wa biashara zao), hivyo hujikuta wanahodhi madaraka yote. Hii inaweza kuchelewesha ukuaji wa biashara zao. Hata hivyo wanapofanikiwa kuongeza mtaji wa biashara zao, ni rahisi kwao kuboresha biashara na kupunguza kuhodhi madaraka. 

3. Kuonyesha ufahari wa kumiliki biashara:  Wenye lengo hili mara nyingi hufuata mkumbo  wa muelekeo wa biashara zinazoonekana kuwa ‘mahiri’ ili waweze ‘kuuza sura’. 
Hawafanyi uchambuzi wa kutosha wa biashara wanazotaka kufanya, na si  wabahiri katika kuwekeza kiasi kikubwa cha fedha ili mradi tuu biashara itajenga na kulinda heshima wanayotaka kuwa nayo. 
Wajasiriamali wa namna hii si watendaji wa kila siku wa shughuli za biashara, hata hivyo hupenda kupata taarifa za mara kwa mara za biashara husika ili nao waweze jidai kwa kundi ambalo wapo. 
Hujali zaidi muonekano wa nje wa biashara kama vile mazingira ya ofisi, vifaa vya kazi, magari n.k, kuliko ubora wa wafanyakazi na kuwaendeleza wafanyakazi. 
Pamoja na kuwa si wabahiri katika kuwekeza katika vitu vinavyoboresha muonekano wa biashara zao, watu hawa wengi wao huwa wabahiri katika kulipa mishahara mizuri kwa wafanyakazi wao, na hawapendi kuona wafanyakazi wakibadilika kimaendeleo.

4. Biashara kama urithi wa baadae: Kwa wengine  lengo la kuanzisha na kufanya biashara ni mchanganyiko wa mambo mawili makuu ambayo ni kutoa mchango kwa jamii na kuboresha hifadhi yao ya mali na fedha. Kwa watu hawa malengo ya muda mrefu ni jambo la msingi sana. 
Pia wapo tayari kujifunza na kujaribu mambo mapya. Wanathamini wafanyakazi wao kuwa ni washirika katika kufikia lengo wanalotaka la kujenga kitu kikubwa katika jamii. 
Biashara kwao sio tuu kuuza bidhaa ili waingize fedha, bali ni kuuza bidhaa zenye kuleta kukidhi mahitaji ya mteja. 
Watu wenye lengo hili kwa kutambua kuwa wateja ndio washirika wao wa kuduma, hujitahidi sana kuwekeza katika mahusiano bora na wateja wao. Hii inajumuisha kujifunza maisha ya wateja, mabadiliko katika maisha ya wateja, kusikiliza malalamiko na mapendekezo ya wateja.
Watu wenye lengo la namna hii, hukakikisha biashara zao zinakuwa na kitu kimoja au (hata zaidi) ambacho kweli ni cha kipekee ambacho siku zote watajivunia nacho na kitadumu vizazi na vizazi, iwe aina yao ya utendaji kazi, bidhaa zenye upekee, mfumo wa uendeshaji wa biashara, au mahusiano na wafanyakazi.
Zaidi sana, watu wenye lengo hili, huwa ni wepesi kutilia maanani mambo madogo madogo ya kitaalamu katika biashara zao, kama vile utambulisho wa biashara zao (rangi za biashara, nembo), mifumo ya mawasiliano ya uhakika, n.k
Mjasiriamali wa namna hii, hana papara wala haraka ya kukuza mauzo yake, bali ana mtazamo wa kuwa na mauzo endelevu na kuona biashara inapanuka siku hadi siku.

HITIMISHO:
Je wewe upo katika kundi lipi ? Inawezekana kabisa mtu kutoka kundi moja kuingia katika kundi lingine.
Share:

0 comments:

Post a Comment