MAMBO 6 YA KUFANYA UPATE AJIRA KWA URAHISI

Pamoja na ukiritimba uliopo katika  soko la ajira, kutokana na rushwa na mambo ya kujuana, bado kuna nafasi kubwa ya wewe kupata kazi unayoipenda na kazi inayolipa. Kabla ya kuanza kulalamika kuwa watu wanapeana ajira kwa kujuana, tafakari kwanza ni kwakiwango gani wewe kama wewe unakidhi matakwa ya waajiri. Wakati wengine wanalalamika kupata kazi Tanzania ni tabu, wapo watu ambao wanabadilisha waajiri wanavyotaka wao, iwe ndani ya Tanzania au hata mipaka ya Tanzania.
La msingi kukumbuka ni kuwa utaajiriwa ili ufanye kazi, tena sio tuu ufanye kazi ili mradi, unatakiwa ufanye kazi kwa ufanisi. Katika makala hii, tunaonyesha mambo 6 ya kuzingatia ili kurahisisha utafutaji wa nafasi ya ajira.
1. Mtandao wako : Kila mmoja wetu anahitaji msaada toka kwa watu fulani. Hivyo hata katika ajira ni muhimu kuwa na mtandao utakaokusaidia kufikia malengo yako ya ajira. Mtandao utakusaidia kwa njia nyingi kama vile kukupa taarifa ya nafasi za kazi , kukusaidia katika kujiandaa na usaili. Pia mtandao wako unaweza kukusaidia katika kukutambulisha kwa waajiri ili kuongeza imani ya waajiri kuhusu wewe. 

2. Uwezo wa lugha ya kiingereza: Kiingereza ni lugha kuu ya mawasiliano katika ajira. Hakikisha una uwezo mzuri wa kuongea na kuandika kwa ufasaha. Hapa tunazungumzia ujue vema kanuni za lugha hiyo kama vile matumizi ya nyakati mbalimbali, viunganishi , n.k , sio tuu kujua kuunganisha maneno mawili matatu. Jizoeze kuandika kwa ufasaha pia. Lugha ya kiingereza itakusaidia kukupa maksi wakati wa usaili (interview). Hali kadhalika uwezo wa kusoma na kuandika kwa ufasaha wa kiingereza utakusaidia katika kufanya kazi kwa uhakika, na hata kuwa mbunifu kwa kujifunza mambo mapya na kuyaelezea.

3. Ujuzi wa uhakika: Kumbuka kuwa sababu kubwa waajiri makini wanakuhitaji ufanye kazi kwao ni kwamba utaweza kuwa mfanisi kwa kile ambacho utatakiwa kukifanya. Hili litawezekana tuu endapo wewe kweli una ujuzi ambao unadai unao, wakati wa kuomba kazi. Kumbuka unaweza kufoji vyeti, ila ujuzi na uzoefu wa kazi, hauwezi kufoji.

4. Uwezo wa kufanya mawasiliano fasaha: Jitahidi sana kufuata kanuni zote za mawasiliano fasaha, ikiwemo kusikiliza kwa umakini  kabla ya kutoa maelezo yako, aina ya mavazi, na muonekano wako. Salamu na ufuatiliaji wa mambo madogo madogo kama kusema ahsante, kufuata maelekezo yote ya matangazo ya kazi kwa ufasaha.

5. Unajitangaza vipi: Katika kutafuta ajira, ni muhimu kuwataarifu waajiri na pia watu wengine kuhusu hitaji lako la kuajiriwa. Hivyo basi jipange vema kuwataarifu ndugu, jamaa na marafiki. Kingine unachoweza kufanya ni kuandaa kazi binafsi zinazotumia ujuzi wako ili watu wakiona kazi zako zilivyo nzuri unaweza kujikuta umepata ajira. Ni muhimu sana kutembelea ofisi za waajiri watarajiwa, ukaomba nafasi ya kuongea na mtu mwenye majukumu ya kuajiri, ili uweze kujieleza au kuacha maombi ya kufanya kazi huko.

6. Taswira uitoayo kwa jamii: Waajiri wako watarajiwa wapo katika jamii unayoishi, na hata wale ambao wanaweza kukufanyia ‘mpango’ ukapata ajira wapo pia katika jamii, hivyo basi ili wakuamini, na wategemee utendaji bora toka kwako ni muhimu uonyeshe kujiheshimu, na kwamba ni mtu unayeweza kuaminika  na kutumainiwa kufanya kazi kwa ufasaha, na kuwa na mahusiano mazuri na wafanyakazi wengine. Angalia aina ya status na picha unazoweka Facebook, Google Plus, au Twitter. Pia kama kuna ka ujasiriamali unafanya sasa, hakikisha biashara yako haiharibu uaminifu na taswira njema kwa jamii.
Share:

1 comment: