MAMBO YA MSINGI KUMSAIDIA KIJANA ALIYEFELI FORM 4

Matokeo ya kidato cha nne (form 4) kwa wanafunzi waliofanya mitihani hiyo mwaka 2012 yameishtua jamii ya watanzania waliopo nchini na waliopo nje ya nchi kwa jinsi ambavyo idadi kubwa ya wanafunzi kufeli ambapo zaidi ya 60% ya watahiniwa walipata divisheni sifuli.
Makala hii inachambua nini kifanyike ili kumsaidia kijana mmoja mmoja aliyefeli :

Tulirahisishe tatizo:
Katika maisha yetu kama binadamu tunapitia magumu mengi na mazuri pia. Magumu kama vile kufeli ni sehemu ya maisha , ingawaje huwa yanatuumiza na wakati mwingine tunakata tamaa. Waswahili wanasema maji yakishamwagika hayazoleki,  hivyo basi kwasasa usiumie kichwa  kwa kuwa umefeli badala yake chukulia hiyo ni changamoto ya kutambua udhaifu wako uliokufanya ufeli, au mapungufu mengine ya kifamilia na kijamii. Kumbuka pia maisha ni zaidi ya kufaulu au kufeli mitihani ingawaje kufaulu kunaweza kukaharakisha kufanya mambo fulani, lakini hakumaanishi wala hakukupi uhakika wa furaha na mafanikio ya maisha. Jambo la msingi ni kwa mtu binafsi kutambua kuwa kushindwa jambo fulani hakumaanisha kuwa jambo hilo haliwezekani . Kijana aliyeshindwa kufaulu mitihani ya mwaka jana, haimaanishi kuwa amefeli maisha. Anayo nafasi ya kujijenga sasa, akafanyia marekebisho yale mapungufu aliyo nayo kwani bado umri unadai, maisha hayajaisha bado, anayo miaka zaidi 20 ijayo kuishi hivyo ajipange na kuandaa maisha yake kwa msaada wa familia, jamaa na marafiki.

Nini cha kufanya sasa:

Kuwa mkweli  : Ni muhimu kwa kijana mwenyewe binafsi kutambua mapungufu yaliyosababisha kutokufaulu mitihani husika. Pengine ni kweli kuna magumu ya kijamii kama vile uhaba wa walimu, au magumu ya kifamilia kama vile hali ngumu ya kifedha, ila hizi ni changamoto tuu ambazo zinaweza kutatuliwa ili kuleta utulivu kwa mwanafunzi. Madhaifu kama vile kutokuwa na bidii ya kusoma, kutafuta misaada zaidi, na kujituma hata pale masomo yanapokuwa magumu.

Kujiboresha  katika English:  Somo la English ni kati ya masomo ambayo ni LAZIMA mwanafunzi alimudu vyema  sio tuu kwa sababu inabidi alifaulu ila English ndio msingi wa kuelewa masomo mengine, kwani mwanafunzi ataweza kujisomea vitabu mwenyewe, na pia kuwa na uwezo wa kuandika majibu kwa ufasaha.

Kujiboresha katika Hesabu:  Kujiboresha katika hesabu ni muhimu , sio tuu kwa sababu hesabu ni somo bali kujiboresha katika hesabu kunamfanya mwanafunzi kuwa hodari katika kufikiria, na kuchanganua mambo. Uwezo wa kufikiria na kuchanganua mambo ni muhimu katika kumuwezesha mwanafunzi kuelewa masomo mengine na hata katika kujieleza.

Kujiboresha katika uwezo wa kutafakari (reasoning):  Hii inawezekana kwa mwanafunzi kujihimiza kusoma kwa umakini na kuelewa, kufanya mazoezi ya mara kwa mara ili kutambua mbinu za ziada za maswali na jinsi ya ujibuji.

Kuamua kusoma kwa ufahamu:  Mwanafunzi anatakiwa aamue kwanza kusoma na kwamba adhamirie kuelewa anachokisoma.Maamuzi haya yanasaidia kumfanya awe na usikivu na kujituma hata pale masomo yanapoonekana kuwa magumu.  Waswahili husema: “huwezi kumlazimisha ng’ombe kunywa maji”.

Hitimisho ni kuwa pamoja na kuwa wengi tunaliangalia tatizo la kufeli kwa wanafunzi kama tatizo la kijamii, makala hii inapendekeza kuwa pamoja na juhudi za jumla za kutatua tatizo hili, kuna haja ya kutafuta njia za kumsaidia mwanafunzi mmoja mmoja. Wazazi na walezi ni muhimu wakae na wanafunzi na kutambua changamoto walizonazo, kuwasaidia mara kwa mara, kwani kufaulu au kufeli mitihani ni matokeo ya maandalizi ya muda mrefu, na kwamba familia, ndugu na jamaa wana mchango mkubwa katika kufanya maandalizi ya mwanafunzi yawe bora.
Share:

0 comments:

Post a Comment