MAMBO 5 YATAKAYOONDOA UVIVU AU KUAHIRISHA AHIRISHA MAMBO YA MSINGI

Baadhi ya watu wamekumbwa na tabia ya kuahirisha mambo ya msingi bila kuwa hata na sababu ya msingi ya kuahirisha huko. Wengine ni uvivu wa kuanza au kuendeleza jambo fulani. Zipo sababu nyingi kwa nini uvivu au kuahirisha huko hutokea. Wengine huwa ni kisingizio maarufu cha kuwa wapo ‘bize’ sana, wakati wengine ni kwa sababu ya kujiachia- yaani kuridhika na hali waliyo nayo sasa (tunasema watu wa aina hii wapo kwenye ‘comfort zone’).
Makala hii inachambua mambo matano (5) ambayo ukizingatia unaweza kushinda uvivu, kuridhika na kuahirisha hairisha mambo ya msingi bila sababu ya msingi:-

1. Weka picha ya maisha mapya: Fikiria vile maisha yako yatakavyobadilika kutokana na kufanikiwa katika jambo ambalo sasa unakuwa mvivu kulifanya au unalifanya kwa kusua sua.  Pengine maisha yako yatabadilika kwa kuongeza mtandao wa watu muhimu katika maisha yako, pengine kipato chako kitaongezeka, pengine jina lako litakua na sifa kwako zitaongezeka, pengine utajitengeneza uhuru wa fikra n.k

2. Tambua wajibu ulionao kwa watu wako wa karibu: Jambo la msingi unaloona uvivu kulifanya au kuliendeleza kiasi kwamba unajikuta unaahirisha mara kwa mara, linaweza kuwa watu walio karibu nawe wanakutarajia ulifanye. Mfano , pengine umetoa ahadi ya kufanya jambo husika, pengine ni jukumu la kikazi, pengine jukumu la kibiashara,  kifamilia, au hata jukumu la kimapenzi (kuwa kufanya kwako jambo husika kutatimiza matarajio ya mpenzi wako).

3.Tambua wajibu wako wa kiroho: Kumbuka pia una jukumu la kiroho la kutenda mambo ya msingi na kuwa mtu wa msaada kwa wanaokuzunguka na dunia kwa ujumla. Haijalishi wewe ni wa dini gani, sote tuna jukumu la kuwa wa msaada kwa wenzetu. Hivyo kama kuanza au kuendeleza jambo unalotakiwa kufanya – iwe kujiendeleza kwako kielimu, kuanzisha biashara,kubadili tabia fulani iwe bora zaidi,  n.k , tambua kufanya hivyo hakutakunufaisha wewe peke yako, bali kutanufaisha wengi.

4.Fikiria ‘maadui’ zako:  Kumbuka kuwa kuna watu ambao wangependa kukuona haufanikiwi, hawa ni ‘adui’ zako. Hivyo kwa kadri unavyoahirisha mambo yako ya msingi au kuwa mvivu katika kuanza na kukamilisha mambo hayo, tambua unatengeneza nafasi za ‘ushindi’ kwa adui zako.

5.Jiambie unaweza: Ukiwa na mashaka ya kuweza kuanza au kuendeleza jambo unalolitamani au kulitafakari itakuwa ngumu pia kuanza jambo husika. Hivyo kujikuta ukiahirisha au kuwa mvivu tuu wa kuanza na kuanza au kuendeleza jambo husika. Watu wengine wanaweza ‘kukupa moyo’ katika jambo fulani, hata hivyo wewe mwenyewe ni muhimu ujione –utengeneze picha ya akilini , kuwa umekamilisha jambo husika kwa mafanikio.
Share:

1 comment:

  1. Asantee maudhui MAZURI mnayochapisha. www.tenachew.com

    ReplyDelete