JINSI YA KUTUMIA FURSA 5 ZILIZOPO KATIKA AJIRA ( UKIACHA MSHAHARA)

Baada ya kumaliza masomo yako, ajira huchukua nafasi kubwa ya maisha yako. Pamoja na ukweli kuwa lengo kuu  la kuajiriwa ni kuingiza kipato, inakubidi utafute namna nyingine za ziada za kufurahia ajira yako zaidi ya kusubiri tuu kupata mshahara mwisho wa mwezi. Mazoea ya kusubiri kufanya kazi kwa ajili ya mshahara tuu, yanaweza kukufanya ukajihisi kuichoka haraka ajira yako, au kujikuta usiye na furaha kazini, ukitilia maanani kuna changamoto nyingi za kifamilia, na kijamii utakazokuwa ukikutana nazo.
Makala hii inachambua fursa 5 ukiacha kupata mshahara. Fursa hizi 5 zinahusu mambo mengine yatakayokufanya uone ajira yako ina maana zaidi ya mshahara unaoupata. Inawezekana ajira uliyonayo sasa isiwe na fursa zote ninazozitaja hapa chini, hata hivyo ni matumaini yangu kuwa ukitafakari kwa umakini unaweza kuambulia fursa walau moja katika hizi zinazoelezwa hapa chini:-

1.Kushiriki katika kumiliki asasi husika: Kuna baadhi ya asasi zina sera ya kuruhusu wafanyakazi kuwa wamiliki wa asasi husika. Pia waweza vutia wamiliki wa asasi uliyopo kukualika uwe mshirika katika umiliki wa asasi yao, kutoka na ufanisi wako wa kiwango cha juu na kujitoa kwako kwa asasi husika. Ili kufanikiwa katika hili, boresha ufanisi wako, jenga mahusiano mazuri na wamiliki, na ujitoe kwa dhati katika kufanikisha mafanikio endelevu ya asasi unayofanyia kazi.Kwako ajira iwe zaidi ya mshahara, bali ni namna unavyoijenga asasi utakayoimiliki hapo baadae.

2.Kujenga mtandao: Unapokuwa umeajiriwa unakutana na watu wa aina nyingi, ukianzia na wafanyakazi wenzako, wateja wa asasi uliyopo, mabosi wako, na wasambazaji wa huduma na bidhaa mbalimbali. Katika makundi yote haya ya watu utaweza kupata wateja wako  wa baadae utakapotaka kujiajiri, pia unapata kujuana na kujenga mtandao wa wasambazaji wa bidhaa na huduma kwako hapo baadae kama vile watu wa benki, wamiliiki au wafanyakazi wa vyombo vya habari, n.k. Pia katika kundi hili unaweza kupata washauri –mentors ambao watakujenga kitaaluma na kuongeza uwezo wako wa kumiliki mambo yako binafsi. Utaweza pia kupata watu ambao wanaweza kuwa wahisani wako wa baadae au watu utakaomiliki nao biashara hapo baadae.

3.Kuboresha ujuzi wako: Ajira yako inakupatia fursa ya kupata ufahamu kwa njia ambazo pengine zingekugharimu sana kama wewe mwenyewe ungekuwa unazilipia. Mfano unaweza kuwa unapata huduma za internet muda wote uwapo ofisini, unapata nafasi ya mafunzo mbalimbali kupitia semina, na hata kozi mbalimbali unazolipiwa ukasome. Tumia vema internet ya ofisi kuongeza pia ujuzi wa mambo mengi ya msingi kielimu na kifikra, na pia kozi au semina unazoenda ziboreshe ujuzi ambao utaboresha utendaji wako hapo ofisini ili upate fursa nyingine zaidi zinazokuja na ajira, lakini pia ujuzi huu utauhitaji utakapokua umejiajiri au umebadili sehemu ya ajira toka asasi ya sasa kwenda asasi nyingine.

4.Kufanya maandalizi ya kujiajiri: Kuwepo kwako katika ajira ni fursa tosha ya kujifunza kwa vitendo jinsi asasi zinavyoendeshwa ili utakapokuja kujiajiri utumie uzoefu na uelewa ulioupata kufanya asasi yako iwe ya mafanikio. Kuna mapungufu utakayoyaona toka katika asasi uliyopo, na mazuri utakayoweza kuiga. Mambo ni mengi unayoweza jifunza toka aina ya nyaraka zinazotakiwa katika kuendesha asasi, jinsi ya kuendesha mikutano mbalimbali ndani ya asasi yako, kanuni na sera zinazofaa katika kuendesha asasi, hadi katika namna ya kujenga mifumo ya ufuataliaji wa maendeleo ya asasi yako utakapojiajiri.

5.Kutengeneza jina kwa ajili ya watu wengine: Ufanisi wako kazini, mahusiano yako bora na bosi wako na wafanyakazi wako, na kwa kupitia mtandao wako utaweza kuja kusaidia watu wengine kupata kazi kwa kuwapendekeza kwa mtandao wako au kwa mabosi wako.  Na kwakuwa tayari umejijengea heshima na uaminifu mbele za watu wengine, ni rahisi kusikilizwa hivyo ukaweza kusaidia ndugu zako, jirani au jamaa mbalimbali kupata ajira kwa mgongo wako.

Hitimisho: Kuzitambua fursa hizi na kuweza kuzitumia vema kunategemea sana na jinsi wewe mwenyewe unavyodhibiti mwenendo wako kazini. Je, una mahusiano ya aina gani na wafanyakazi wenzako, bosi wako, na wateja wa asasi yako ? Je, unabidii kiasi gani ya kujifunza mambo mapya ukiwa kazini, je una ufanisi wa kiwango cha juu katika utendaji kazi ? Je, unakabiliana vipi na changamoto unazokumbana nazo? Je unaheshimu vipi taratibu na sera za asasi uliyopo? Je unajua kiwango gani cha ufanisi unatazamiwa kuwa nacho hapo kazini kwako ? Je, wajua majukumu yako na unayatekeleza kwa kiwango gani ? n.k
Share:

0 comments:

Post a Comment