SABABU 5 KWANINI UPENDO HAUTOSHI KUJENGA MAHUSIANO BORA

Ukisoma kwa kutafakari makala hii utagundua kuwa kuweza kujifahamu sisi wenyewe vema, kuweza kujitawala sisi wenyewe, na pia kuweza ‘kuwasoma’ vema wenzi wetu , ni mambo ya msingi sana ili upendo tulionao uweze kudumisha mahusiano.  Msisitizo ni kwamba, pamoja na ukweli kuwa upendo ni kitu cha muhimu katika mahusiano, makala hii inaeleza kuwa kutegemea upendo pekee kama nguzo kuu ya mahusiano bora kunaweza kuwa jambo la hatari kwa mahusiano, kwa sababu zifuatazo:-

1. Binadamu ni kiumbe huru: Ni muhimu kukumbuka hili hasa kama unadhani kwakuwa unampenda fulani na umemuonyesha mapenzi yako yote basi hicho ni kama kifungo kwake kuwa hatoweza kutoka katika penzi lenu. Kwa asili binadamu ni huru, na anaweza kuamua kuutumia uhuru wake kufanya maamuzi mengine yoyote tofauti na unavyofikiri ni lazima afanye.  Kwa kuwa pia ni mbinafsi, basi kama upendo wako wote kwake hauendani na yale anayotazamia , unaweza kukuta ameshindwa kukaa katika penzi , ambalo kwa watu wengi wanaona kuwa ni penzi zito.

2. Binadamu ni mbinafsi kwa asili: Binadamu kwa asili huangalia maslahi yake kwanza kabla ya kuangalia ya mwingine. Mfano dhahiri wa ubinafsi huu ni pale inapotokea ajali , mara nyingi mtu huwaza kujiokoa mwenyewe kwanza kabla ya kufikiria wa karibu yake. Tumesikia habari za mama mzazi kuacha kitoto kichanga ndani wakati moto ukiendelea na yeye kutoka nje. Kuna habari pia za mama kumtumia mtoto wake kama ‘kifaa’ cha kuvunjia kioo cha gari , ili aweze kujiokoa, pale ambapo ajali ilitokea. Hivyo upendo tuu pekee hautoshi kumfanya mtu aendelee kukaa katika ndoa au mahusiano kabla ya ndoa (uchumba), ni muhimu yawepo mambo mengine yenye manufaa kwa mtu husika.

3. Binadamu ana mahitaji mengi  na yasiyo na kikomo:  Mwenza wako ana mahitaji mengi na yanaongezeka na kubadilika siku hadi siku kutegemeana na mabadiliko mbalimbali kama vile hali ya hewa, aina ya kazi,  watu anaokutana nao, mabadiliko ya teknolojia, mabadiliko ya kiuchumi n.k. Upendo wenu, hausimamishi mahitaji haya yasitokee, na kwamba upendo pekee hauwezi kuwa jibu la kutimiza mahitaji hayo. Inahitajika bidii katika kujituma kujiletea kipato, kuwa na mawasiliano bora kati yenu, kutambua mabadiliko na kuchukua hatua kabla mabadiliko hayajawabidilisha, na zaidi sana muweze kuwa na utamaduni wa kupanga mambo pamoja na kuwa waaminifu katika kutimiza yale mnayopanga. 
Chukulia mfano, wa wanandoa walioishi vema kwa miaka 5 ya ndoa, halafu ndoa ikaanza kulemaa kwa kuwa mmoja wao anaona hakuna uwajibikaji katika kumsaidia mwengine kujiendeleza kielimu, kibiashara, au kutimiza ndoto nyingine ambayo mwanandoa amekuwa nayo.

4. Binadamu wengi wanashindwa kujitawala:  Uwezo wa mtu kujitawala unaweza ukakinzana na upendo wake kwa mwenza wake, hivyo kuleta hali ya kutoridhika kwa mwenzi wake, kitu ambacho kinapunguza  au pengine hata kuondoa raha ya mahusiano. 
Mfano utakuta kwa kufuata makundi ya marafiki aliyonayo, mwanaume anakuwa mlevi wa kupindukia,  na kujikuta akiingia katika anasa na maamuzi mengine yasiyo mazuri kwa mpenzi wake na familia kwa ujumla. Hata hivyo mwanaume huyo huyo ukimuuliza kama anampenda mke wake au la, atakujibu anampenda sana. Tatizo nini ? Utajibiwa, ni pombe tuu ndio mmemtawala, na kwamba jamaa ana ‘kampani’ mbaya.

5. Maana isiyo sahihi ya upendo: Kuna wengi wanaodai wanao upendo lakini kiukweli walichonacho sio upendo bali ni tamaa au matakwa ya kuhitaji kutimiziwa mambo fulani. 
Maana halisi ya upendo sio vile unavyotaka fulani akufanyie mambo au jambo fulani, upendo sio vile unavyojisikia baada ya fulani kukutendea jambo uliloliona jema kwako, upendo sio vile fulani anavyokufanya ujisikie kwa sababu ya sura yake au umbo lake, BALI, upendo ni utayari wako wewe kufanya mambo yanayompendeza mwingine, kuwa tayari kuona mwingine ana furaha juu yako.  
 Kwa maana rahisi , upendo si jambo linalokuhusu wewe unajisikiaje, bali ni vile unavyotaka mwingine ajisikie.
Kwa maana nyingine, utatimiza vema upendo wako kwa kujitahidi kumfahamu mwenza wako, kutimiza yale anayohitaji (ili awe na furaha) sio kutimiza yale unayotaka wewe kwa makusudio yako binafsi. Upendo unahitaji kumheshimu mwenza wako, kumsikiliza, kumfanya akuamini, na aendelee kukuamini.
Pamoja na kuwa hisia za kimwili (chemistry) ni muhimu sana katika kujenga mahusiano yenu,  hisia za kimwili zisichanganywe na upendo. 
Kwakuwa fulani amekuvutia kimwili haina maana kuwa basi unampenda mtu huyo. 
Kufanya tendo la ndoa, sio lazima iwe ndio ishara ya uwepo wa upendo katika yenu, kwani wapo hata wanaofanya tendo la ndoa kama biashara.

Hitimisho
Mahusiano hususani mahusiano ya kimapenzi yanatutaka tuwe waajibikaji kwa wenzetu, na kwetu wenyewe. Kuwajibika kwa wenzetu ni pale tunapojifunza vya kutosha tabia,  na yale yanayompendeza na yasiyompendeza mwenza wetu. Wakati tunawajibika kwetu wenyewe kwa kujifunza kuhusu mapungufu yetu, na kujituma kujirekebisha. Mapenzi yanaleta majukumu, na bila kutambua na kutimiza majukumu husika, mara nyingi mapenzi yatageuka kuwa karaha, badala ya furaha.
Share:

0 comments:

Post a Comment