MABADILIKO SITA (6) DUNIANI USIYOPASWA KUPUUZIA

Pilika zetu za kupata fedha, vyeo, kujenga mahusiano na kukubalika katika jamii zinaathiriwa na mabadiliko yanayoendelea kutokea katika jamii yetu. Makala hii inadokeza mabadiliko 7 muhimu kuyafahamu na kuyatawala ili usije kujikuta unapoteza furaha ya kweli ya kuishi kwa kuwa mtumwa wa fedha, mapenzi, cheo, mahusiano au mtumwa wa ‘misifa’.

1. Uhuru wa mawasiliano: Uwepo wa mitandao ya kijamii, kushuka kwa bei za simu na kompyuta , teknolojia ya upigaji picha na uandishi kama vile kutumia blogs, ni baadhi ya mambo yanayochochea uhuru wa mawasiliano kukua. Uhuru huu unaweza athiri malezi ya watoto,  uhuru pia unaweza athiri usiri wa mambo yako, na bila shaka unaathiri ufanisi wako kibiashara na kikazi pia.
Ili kuweza kujitawala na kutawala mabadiliko haya ya uhuru wa mawasiliano, inakupasa ujifunze vema matumizi ya teknolojia husika, au upate mtu wa kukusaidia kusimamia mambo yako ili yasiathirike na uhuru huu wa mawasiliano.
Fahamu yapi unastahili kufanya ukiwa mtandaoni – kwa simu na kwa kompyuta, tambua pia nini watu wanafanya ambayo yanaweza  kukuathiri.  Mfano mzuri,  ni pale unapoweka picha ya mpenzi wako aliyependeza vizuri, ila picha hiyo ukaikuta imewekwa kwenye mitandao ya ngono.
Mfano mwingine, usipofuatilia mara kwa mara anachoandika mtoto wako mtandaoni unaweza kushtushwa siku ukawa tagged picha binti yako aliyepo ‘boarding school’ akila ‘bata’ kwenye club ya usiku. Au kukuta ameandika status – “ Jamani, siwezi soma huyu BF wangu kila nimfanyiacho haridhiki, nimempa hadi  pocket money zangu akae nazo, ila haridhiki”.

2. Machafuko katika jamii:   Hali ngumu ya kiuchumi, mabadiliko katika uwezo wa kifikra wa watu, na ukandamizaji uliokithiri katika jamii zetu ni moja ya sababu zinazochochea machafuko ya kila siku yanayoendelea. Hata yale ambayo ulidhani kuwa hayawezi kutokea nchini mwetu, bila shaka utaanza kuyaona yakitokea. Hali hii ni muendelezo wa mabadiliko makubwa katika maisha yetu. Serikali zinazidi ‘kuchangikiwa’  kwakuwa mabadiliko yanatokea kwa haraka sana na ni mabadiliko makubwa ambayo hayakutazamiwa. Hivyo  serikali kujibu mapigo haya, inabidi zije na mbinu nyingi kali zinazoweza kuonekana kama ni za kidikteta.

3. Uzalishaji mkubwa wa ushindani wa hali ya juu:  Kupanuka kwa fikra za watu wengi, maboresho katika teknolojia, urahisi wa upatikanaji wa taarifa, na mijumuiko ya watu toka mataifa tofauti katika nchi tofauti,ni mambo yanayoleta ushindani katika uzalishaji. Mbinu zilizosaidia biashara fulani kuwa kubwa miaka 10 iliyopita, zinaweza zisiisaidie biashara hiyo hiyo, au nyingine inayofanana nayo kukua.
Wajasiriamali sasa wanazalisha bidhaa mpya, ubora unaboresha, bei zinazidi kuenda chini, na mbinu za kufikisha bidhaa kwa mteja zinaboreshwa.  Mabadiliko haya, yanahitaji mjasiriamali sio tuu ajue vema kuzalisha bidhaa yake, ila aifahamu vema jamii anayotaka kuiuzia bidhaa, ajenge mtandao mkubwa na wateja wake, na zaidi sana aweze kukusanya na kusimamia taarifa za jinsi ya kuboresha ushindani wake katika soko.

4.Utitiri wa taarifa:  Maboresho katika teknolojia ya habari na mawasiliano, yamechangia sio tuu kuwepo kwa websites na mitandao ya kijamii (social networks) bali yamerahishisha matumizi na hata umiliki wa mitandao. Mfano kuna blog kibao Tanzania pekee, na kurasa maelfu za Facebook. Kuna video mamilioni kwenye Youtube.
Usipoweza kutawala vema hali hii ya utitiri huu wa taarifa unaweza kujikuta unakuwa mtu wa kupotoshwa, na mtu usiye mfanisi katika mambo yako ya kielimu, kikazi na hata kibiashara. Hakuna wakati unaohitaji ujuzi wa kipekee wa kutawala muda wako, na pia kuweza kuchambua taarifa unazozipata.

5. Maboresho makubwa katika teknolojia mbalimbali: Si tuu upande wa teknolojia ya habari, bali aina nyingi za teknolojia kama vile teknolojia za uzalishaji wa vyakula na teknolojia za utengenezaji wa mashine.  Mambo haya si tuu yanaleta bidhaa mpya na kubadilisha mfumo wa uendeshaji wa mambo mengi, pia yanaleta athari nyingine ambazo inatupasa kuwa makini nazo kama vile, athari za kiafya , athari za malezi (kuporomoka kwa maadili), athari za kiuchumi (biashara nyingi kuporomoka kwa kushindwa kushindana).

6. Uharaka wa usambaaji wa mabadiliko:  Kwa jinsi dunia ilivyo ‘kijiji’ mabadiliko yanayoendelea makubwa ya kiuchumi, kiteknolojia, kisiasa , na kijamii yanaathiri si tuu taifa moja ambapo badiliko fulani limetokea, bali mabadiliko hayo husambaa kwa haraka kwa nchi nyingine. Kama ilivyo kwenye usambazi wa bidhaa mbalimbali unavyosambaa kwa haraka – kumbuka matoleo kadhaa ya simu kama iphone, Samsung, n.k yanavyofikia Bongo, tutarajie mabadiliko mengine yanayotokea nchi za maghariba na barani Asia kufika kwa haraka hata Tanzania.

Hitimisho: Elimu ya darasani pekee haitoshi kukusaidia kupita na kutawala mabadiliko haya makubwa, unahitaji kupenda kusoma ziada.
Hakikisha unapata taarifa sahihi kwa kufuatalia kuaminika kwa chanzo cha taarifa. Pia tumia search engine kama Google, kutafuta vyanzo vingine vya habari vinasema nini kuhusu taarifa unayodhani ni sahihi.
Linda sana utashi wako kwa kuwa huo pekee ndio mali kubwa zaidi kwa maisha yako. Ukipoteza utashi wako kwa tamaa ya mali, kufuata mkumbo n.k utajikuta unapotea zaidi.
Kuwa tayari kubadilika kuendana na mazingira na hali halisi – elimu, aina ya biashara, aina ya kazi, mahali pa kuishi, mahusiano, malezi ya watoto.
Katika nyakati tulizopo,  ni muhimu sana kuufahamu na kuuishi msemo huu “ Don’t  Work Hard, Work Smarter”yaani “ Usifanye tuu kazi kwa nguvu zako zote, bali fanya kazi kwa akili zaidi”.
Share:

0 comments:

Post a Comment