ELIMU ILIVYO MZIGO KWA WENGI WETU

Pamoja na kuwa elimu ni kitu muhimu sana maishani, kwa watu wengi kitu elimu kimekuwa ni mzigo mkubwa kiasi kwamba badala ya kuboresha maisha, elimu imekuwa ikirudisha nyuma maendeleo. Badala ya elimu kumsaidia mtu kuwa na furaha , inamletea huzuni. Pia, si ajabu kukuta mtu mwenye ‘elimu kubwa’ au tumuite ‘msomi’ akifanya mambo ambayo hakutarajiwa kufanya. Makala hii inachambua mambo ya msingi ya kuangalia ili elimu isiwe mzigo kwako:-

Inatuweka njia panda:  Imani kuwa kiwango fulani cha elimu ndio msingi wa ‘kutoka’ kwako kimaisha, yaweza kukufanya ukaacha mengi ya msingi ambayo ungeweza kufanya na kufanikiwa kimaisha, badala yake ukajikuta unataka KWANZA upate kiwango hicho cha elimu unachodhani ukikipata ndio utaanza ‘kuishi’.  
Ingawa ni kweli kuwa elimu ni muhimu, hasa viwango vya juu vya elimu ni muhimu katika kukurahisishia kuongeza fursa mbalimbali, haina maana kuwa mafanikio yanapatikana kwa njia pekee ya kuwa na elimu ya kiwango kikubwa. Hivyo basi unapojikuta upo katika njia panda ya kuchagua kufukuzia kwanza kiwango fulani kikubwa cha elimu, hakikisha unawaza  na kutafuta njia nyingine mbadala za kupanua fursa mbalimbali kwa kutumia kiwango ‘kidogo’ cha elimu ulicho nacho. 
Uwe na mtazamo wa kuwa mzalishaji, mtu mwenye furaha , na unayeishi kwa namna ile uwezayo kweli kweli, sio kwa kufuata matarajio ya watu wengine. Kwani baadhi yetu hujikuta tunajikita na elimu kwa kuwa tuu hivyo ndivyo ndugu zetu , marafiki zetu, au familia inavyotegemea tutafanya. Au kwa kuwa unataka kushindana na watu fulani. Usiwe mwoga wa kutokuendana na matarajio ya watu wengine. Weka matarajio yako, na jiamini kuwa utayatimiza.

Inagharimu uhuru wa watu:  Kwa baadhi ya watu, elimu badala ya kuwaweka huru, inawafanya watumwa wa kifikra kwa namna mbalimbali, kama vile kuamini tuu kila aliyesoma sana anachosema ni sahihi, kuamini kuwa fani yake ya elimu ndio suluhisho pekee la matatizo au changamoto fulani, mfano mchumi kuamini kuwa matatizo ya ajira yatasuluhishwa na mbinu za kitabuni za wachumi waliopita.  
Elimu pia inaweza kumfanya mtu ajishushe thamani au ajione hafai kuwa na mtazamo tofauti na yule anayemuona kuwa amemzidi ‘elimu’, hata kama ni kweli kwa mtazamo huru , huyo anayeonekana kuwa ‘msomi zaidi’ anakosea, ila kwa kuwa tuu ana elimu zaidi, basi wengine inabidi wajishushe na kukubaliana nae. Ni kama vile kusema “mkubwa siku zote hakosei”. 
Tumedokeza pia, hamasa kubwa ya kutaka kiwango fulani cha elimu inaweza kumnyima mtu ‘uhuru’ wa kuangalia fursa nyingine za kimaendeleo.

Inarudisha nyuma uwezo wa kufikiri:   Elimu inarudisha nyuma uwezo wa kufikiri kwa baadhi ya watu hasa pale inapoleta uwoga wa kuwa na mtazamo tofauti na ule ambao mtu tayari ambaye anatambulika kuwa ni ‘msomi’.  Hatari zaidi ni kuwa baadhi ya watu huogopa kuwa na mtazamo tofauti na ‘ukweli’ ambao amefanya kuusikia tuu.
Pia kwa wale waliogemea sana fani zao, hujikuta wakitafsiri kila kitu kupitia fani zao, na hata kama haviendani  na hali halisi, wao huona ni sawa.  Hii ni kwakuwa kwa baadhi ya watu, elimu inaleta kujiaminisha usahihi wa wayafanyayo au wa yale wafanyao wengine wenye elimu fulani.
Inafanya watu wajitenge : Kwa baadhi ya watu, kiwango fulani cha elimu ndio utambulisho wa thamani ya mtu, na pia ndio  tiketi ya kukubalika kwake au kuwakubali watu wengine. Si ajabu basi kukuta mtu mwenye wazo zuri la kimaendeleo, akipuuzwa kwakuwa tuu , kiwango chake che elimu hakidhihirishi asemacho ni sahihi, yaani “hafanani” na anachosema. Utasikia mtu akimwambia mwenzake bila haya “ mi siongei na wasio soma”.

Inakosesha fursa:  Kwa sababu elimu kwa baadhi ya watu ni chanzo cha kutokuwa na uhuru wa kufikiri, kwakuwa elimu inawapelekea watu hao wawe wazito katika kufikiri kwa ufasaha,  kwa kuwa pia inawafanya watu wajitenge kwa kuwa na dharau, upo uwezekano wa elimu kuwakosesha fursa baadhi ya watu.

Hitimisho
Lengo la makala hii haikuwa ‘kuponda’ elimu au ‘wasomi’, bali kusisitiza kuwa elimu inafaa ilete manufaa kwetu. Na hivyo pale unapohisi inaleta mambo tuliyotaja hapo juu, au yanayofanana na hayo basi ni wakati wako kubadilika, au kutafuta msaada wa jinsi ya kurekebisha hayo. La msingi sana ni kuhakikisha kuwa elimu, pamoja na uzuri wake, haichukui nafasi ya ubinadamu wako, utashi wako na nguvu yako kubwa ya kufanya maamuzi.
Elimu ikusaidie kuona uhalisi katika uhalisi wake, sio ikuonyeshe hali tofauti na kukuaminisha kuwa ndio hali halisi.
Unalo jukumu la kuitawala elimu, na sio elimu ikutawale wewe, hii inamaanisha kuwa sio kila kitu utakachosoma utalazimika kukiamini, na kwamba uwe tayari kukubali kuwa mambo fulani uliyoyasoma na ukayaamini wakati fulani yanaweza yasiwe sahihi wakati mwingine hivyo ikakubidi utafute uelewa mbadala.
Share:

0 comments:

Post a Comment