BUSARA HII KATIKA MATUMIZI YA MUDA INA MANUFAA MAKUBWA

Kuna  sababu nyingi zinazotofautisha watu waliofanikiwa na wasiofanikiwa, lakini zaidi sana sababu ya utofauti huo ipo katika MUDA. Ndio, sababu ni MUDA,  muda toka mtu ameamua kutenda anayohitajika kutenda ili afanikiwe, muda ambao mtu anaweza kuvumilia, muda ambao mtu ameamua kupoteza bila kuwa na mkakati maalum, muda unaotumika kufanya jambo la msingi, Muda wa kusubiria wakati muafaka wa kufanikiwa kwako utimie n.k. Makala hii inachambua namna unavyoweza kujiongoza vema kutumia muda ili kuleta mabadiliko chanya katika maisha yako.

Jambo la msingi zaidi kwanza: 
Hii inaonekana ni rahisi kusema kuliko kutenda kwa sababu wengi wetu hukumbwa na kigugumizi katika kutambua jinsi ya kupanga mambo yetu kwa ngazi za umuhimu ili lile la muhimu zaidi au la msingi zaidi lianze. Matokeo yake ni kujikuta tunatumia muda mwingi kufanya mambo machache yasiyo na uzito mkubwa kwetu,  na kuyapa muda mdogo yale mambo yaliyo na uzito hasa kwetu. Kanuni rahisi ya kukuweza kupanga mambo kwa ngazi za umuhimu ni kupima mambo kwa vigezo vifuatavyo:-

Uwezekano wa kuhairisha jambo: Je ni lazima jambo husika lifanyike muda huu ? Je inawezekana kuliahirisha na kufanya baadae ? Je athari za kuahirisha ni zipi ?
Linganisha faida za sasa na za baadae : Je, jambo hili na lile lipi litakunufaisha zaidi sasa ? Je lipi litakunufaisha baadae ? Pia linganisha faida ya sasa na faida ya baadae, jambo lipi linakupa faida zaidi?
Linganisha rasilimali zinazotakiwa kutumika : Jiulize jambo lipi linatumia zaidi rasilimali kuliko nyingine, na je unaweza kufanikisha kwa ufanisi zaidi jambo gani kwa kutumia rasilimali unazoweza kupata.
Hivyo basi , kanuni hii ya kufanya jambo la msingi zaidi kwanza, inatuhitaji tusiwe watu wa kukurupuka, badala yake tuwe wachambuzi wa maisha na yale tunayokumbana nayo ili tujipange vema. Wengi wetu hujipa moyo kwa kusema, “aah lakini hili jambo nifanyalo ni la muhimu”. Wakati kinachotakiwa ni kufanya ‘la muhimu ZAIDI’

Muda ulivyo tabibu: 
Kuna msemo usema “ unaposhinda, mheshimu uliyemshinda,  na unaposhindwa pia mheshimu aliyekushinda”.  Msemo huu una maana kubwa sana kuwa muda ni dawa au tabibu wa mambo mengi. Wapo wengi waliokuwa matajiri wameporomoka, na wapo wengi waliokuwa masikini wamekuwa matajiri. Hivyo kwa wewe uliye katika hali duni , usijione kuwa basi hapo ulipo ndio mwisho. Kumbuka muda ndio kila kitu, na kwakuwa muda bado upo, wewe unao uwezo wa kubadilika na kuwa juu, ukiweka nia, na juhudi ya dhati.  Kwa wewe ambaye upo na maisha ya kuridhisha, usiwadharau wengine, hata wewe ni muda tuu ndio unakufanya ujihisi hivyo ulivyo. Huu ni muda wako, kwani hata wewe , au waliokufanya hapo ulipo nao walikuwa na muda wa kusota.

Kila jambo ni tokeo la juhudi na muda uliotumika:  Kutana na bwana PM, mwenye umri wa miaka38, kwa sasa anasoma masomo ya ngazi ya cheti  katika chuo kimoja binafsi jijini Dar es salaam. Bwana PM alipomaliza kidato cha nne, hakufaulu, na hakukuwa na uwezo katika familia yake ya kumpeleka masomo ya ziada. Alikaa mtaani kwa miaka kadhaa ,kisha baadae akapata kibarua na kufanya kazi kwa miaka kadhaa. Mara kwa mara alijikumbusha azma yake ya kujiendeleza, lakini kila wakati akawa akijiambia hayupo tayari. Miaka imepita na sasa ana familia ya watoto wawili, kisha anafikiria kuwa inabidi aonyeshe mfano kwa watoto wake kwa kujiendeleza kusoma.  Alifanya mitihani ya ku resit na akapa credit za kumfanya aendelee masomo ya cheti. Bwana PM amefikia hapo alipo kwa juhudi zake mwenyewe na muda alioutumia. Kama angefanya maamuzi mapema ya kuanza kujisomesha, hivi leo angejikuta yupo mbali, kwani yeye mwenyewe anasema miaka 6 nyuma alikuwa anapata kipato cha kutosha kujiendeleza kusoma, ila alidhani hakuwa tayari kusoma.

Picha kubwa ya maisha:
Fikiria kwa muda mfupi, aina gani ya maisha ulikuwa ukipenda uishi, je ni hayo uliyo nayo sasa. Je, unadhani hapo ulipo ndipo ambapo ulitamani kuwa miaka 5 au 10 iliyopita? Je, mke au mume , au mpenzi uliye naye, ndio wa aina ile uliyowahi kuifikiria na kujiambia kuwa utakuja kuwa na mtu wa aina hiyo ? Majibu kwa walio wengi wetu ni kuwa, vile tulivyo leo, vitu au watu tulionao karibu, maeneo tunayoishi, kazi tunazofanya, n.k sio vile ambavyo tuliwaza kuwa navyo. 
Hata hivyo, sio kwamba maisha yamefikia mwisho. Hata kama hatujafikia vile tuliwaza au kutamani kuwa, ni wazi kuwa maisha yanaendelea, na tuna imani ya kufanya makubwa zaidi. Hili ni somo kubwa sana kuwa hatuna haja ya kujiona ni bora zaidi ya wengine, kuwadharau wengine, au kuwakatisha tamaa wengine hasa pale tunapodhani   ‘tumekwisha toka kimaisha’ kwakuwa hata hivyo tulivyo leo sio kwamba tulifikia kwa mikakati au formula ya aina moja. Pengine tunao waona wapo chini yetu, ni kwamba nao wanapitia na kujaribu mikakati fulani fulani ambayo mingine itafanikiwa, mengine haitofanikiwa. Wengine hawafanikiwi kwa sababu ya watu kama wewe unayewaangalia walio chini yako kama  ‘washindani ‘ wako kimaisha, wakati kiukweli  kila mtu ana picha ya peke yake ya kutoka kimaisha.

Imani na matendo:
Jambo la msingi ni kuamini kuwa unaweza kutimiza hilo unalolitaka. Imani peke yake haisaidii, fanya matendo hasa yanaendeana na imani yako. Huwezi kumkuta padri anaswalisha msikitini wala shekhe anaswalisha kanisani, kwakuwa Imani na Matendo havitokuwa sawa, hivyo basi usitegemee kama imani yako ni kufanikiwa, lakini matendo yako – ikiwa pamoja na kule kusoma kwako, mikutano yako na aina ya watu ulio nao karibu haviendani na yale unayotamani kuwa.
Share:

0 comments:

Post a Comment